Trending News>>

Kinacho endelea katika uokoaji wa miili Ziwa Tanganyika


Baada ya kuokoa miili 19 ya watu waliozama katika Ziwa Tanganyika mkoani Kigoma, Jeshi la Polisi kupitia kwa Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani humo Switibert Njewike, limesema kazi ya uokoaji bado inaendelea.

Njewike ambaye ni Kamishina Msaidizi wa Polisi amesema wanatafuta miili mingine 3 ili kutimiza idadi ya watu 22 ambao wanakadiliwa kuwa walikuwemo kwenye mtumbwi ambao uligongwa na boti na kuzama majini.

“Kazi ya uokoaji inaendelea, hadi jana tumefanikiwa kuokoa miili 19 na tunaendelea kutafuta miili mingine mitatu ili kufikia idadi ya watu 22 kama ambavyo makadilio ya awali yalieleza kuwa mtumbwi huo ulibeba watu 22”, amesema Kamanda Njewike.

Kwa upande mwingine Kamanda Njewike amewataka madereva wa vyombo mbalimbali vya usafiri nchi kavu na majini ikiwemo Mitumbwi, bodaboda na magari ya abiria kuzingatia sheria za usafiri na usalama barabarani ili kuepusha ajali hususani kipindi hiki cha sikukuu.

Ajali hiyo ilitokea usiku wa kuamkia Ijumaa ikihusisha boti iliyokuwa inatoka Kigoma mjini kwenda Kalya na mtumbwi wa MV Pasaka uliokuwa ukitoka kijiji cha Kalilani kwenda Sunuka.

No comments:

Powered by Blogger.