Kusambaa kwa picha inayomuonyesha Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri
(DED) ya Ubungo, John Kayombo akiwa amevalia sare za CCM kumeibua
mjadala wa kimaadili huku Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ukieleza
kutishika iwapo kutakuwa na matokeo chanya katika uchaguzi.
Picha hiyo inayosambaa katika mitandao ya kijamii inamuonyesha Kayombo
akiwa katika mkutano wa uchaguzi wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM)
uliofanyika hivi karibuni huko Dodoma akiwa amevalia sare za chama hicho
tawala huku kishangilia.
Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni katika Ofisi ya Rais -
Utumishi na Utawala Bora, Ruth Mollel amesema mtumishi wa umma anatakiwa
kuwa ‘neutral and impartial’ (asiyependelea upande wowote na mwenye
maadili) na awe tayari mara zote kutekeleza sera za Serikali ya chama
chochote.
Ruth aliyewahi kuwa katibu mkuu wa Utumishi, alisema lengo la dhana hiyo
ni kuifanya sekta ya utumishi wa umma kuwa endelevu na kuepuka
mabadiliko ya watendaji wakuu kila Serikali ya chama tofauti inapoingia
madarakani.
“Serikali ya Awamu ya Tano imekiuka dhana hiyo kwa kuingiza siasa katika
utumishi wa umma. Tumeshuhudia nafasi za utendaji serikalini zikitolewa
kwa makada na wakereketwa wa CCM ambao baadhi hawana hata ufahamu wa
uendeshaji serikalini,” alisema.
“Tumeshuhudia naibu katibu mkuu wa Tume ya Mipango akigombea ubunge wa
Bunge la Afrika Mashariki, huku akiwa bado mtumishi wa ngazi ya juu
serikalini.”
Alisema jambo alilofanya mkurugenzi wa Ubungo linaashiria uteuzi mbovu
uliofanywa na mamlaka na kwamba, una lengo la kuvuruga chaguzi
zitakazofanywa.
Ruth alisema tayari dalili zimeshaanza kujionyesha katika chaguzi ndogo zilizomalizika hivi karibuni.
Katika hotuba aliyoiwasilisha katika Bunge la Bajeti la mwaka 2017/18,
Ruth alisema kati ya wakurugenzi watendaji 195 walioteuliwa hivi
karibuni, 65 walikuwa wagombea wa ubunge kwenye kura ya maoni ya CCM,
huku baadhi ya makatibu tawala wa mikoa na wilaya na makatibu wakuu ni
wakereketwa wa chama hicho.
“Matokeo ya uamuzi huu ni kuingiza siasa katika utumishi wa umma na
kupoteza weledi na ni kupanda mbegu mbaya ya ubaguzi wa kisiasa katika
utumishi wa umma,” alisema.
Alihoji, “Inakuwaje kwa mfano, chama kingine kikichukua madaraka ya
dola? Hali ya watumishi wenye itikadi tofauti itakuwaje? Je, naibu
katibu mkuu wa Tume Mipango ambaye kura zake hazikutosha katika kugombea
ubunge wa Afrika Mashariki amerudi kazini?”
Alisema kambi ya upinzani imesikitishwa na kitendo cha mkurugenzi
Kayombo kuuonyesha wazi umma anachokiamini jambo ambalo ni kinyume cha
utawala bora.
Alitoa mfano alipokuwa mtumishi wa umma hakuonyesha mapenzi yake kwa kuwa aliamini anawatumikia Watanzania na si wana CCM.
“Serikali iache mara moja kuteua au kuajiri watumishi kutokana na
itikadi za kisiasa na badala yake ijenge utumishi wa umma wenye weledi
ambao uhai wake hautegemei chama kilichopo madarakani, bali utumishi wa
umma endelevu unaotumikia wananchi,” alisema.
Alipotafutwa kutoa ufafanuzi kuhusu picha yake kuonekana mitandaoni,
mkurugenzi Kayombo alijibu kwa kifupi kuwa hajui lolote na ndiyo kwanza
alisikia habari hizo kutoka kwa mwandishi wetu.
“Sijui lolote yaani ndiyo nasikia jambo hili kutoka kwako,” alisema Kayombo.
Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Ramadhani Kailima
akizungumzia nafasi za wakurugenzi wa halmashauri ambao ni wasimamizi wa
uchaguzi wa majimbo, alisema kwa mujibu wa kanuni ya 16 ya kanuni za
uchaguzi wa Rais, wabunge na madiwani za mwaka 2015 pamoja na kanuni ya
12 ya kanuni ya Serikali za Mitaa (uchaguzi wa madiwani) za mwaka 2015,
kila mratibu wa uchaguzi au msimamizi msaidizi wa uchaguzi kabla
hajaanza kutekeleza majukumu yake wakati wa uchaguzi atapaswa kufanya
mambo matatu.
“Kwanza anapaswa kula kiapo cha kutunza siri katika fomu namba sita;
kula kiapo cha kujitoa uanachama wa chama cha siasa iwapo ni mwanachama
katika fomu namba saba; au kula kiapo cha kusema si mwanachama wa chama
chochote cha siasa katika kipindi cha utekelezaji wa kazi za uchaguzi
katika fomu namba saba,” alisema.
Pamoja na maelezo hayo ya Kailima, mwanasiasa mkongwe, Njelu Kasaka
alisema hakuna mipaka kati ya utumishi wa umma na watendaji wakuu kama
wakurugenzi na makatibu wakuu wa wizara.
Kasaka aliyekuwa miongoni mwa wabunge 55 walioasisi kundi la G55
lililotaka kuundwa Serikali ya Tanganyika mwaka 1993, alisema
hashangazwi na vitendo vinavyoendelea ambavyo kwa mtazamo wake si sawa.
“CCM ilimpokea Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Profesa Kitila Mkumbo na hakuna mamlaka yoyote inayokemea vitendo hivyo,” alisema.
Kasaka alisema, “Ninachojua mtumishi wa umma wa ngazi za juu haruhusiwi
kujionyesha waziwazi kama yeye ni kada wa chama kindakindaki labda kama
sasa mambo yamebadilika kwa sababu sipo huko muda mrefu, kama wamebadili
naweza kusema ni sawa ila kama yapo vilevile kama nilivyoyaacha hiyo si
sawa.”
Mwananchi.
Chadema wahofia uchaguzi 2020...
Reviewed by Unknown
on
December 17, 2017
Rating: 5
No comments:
Post a Comment