Trending News>>

MAWAKILI wa Godbless Lema Wahaha

GODBLESS Lema Mbunge wa Arusha Mjini yuko mbioni kutoka mahabusu. Ni baada ya kukaa mahabusu kwa siku 50 tangu alipotiwa mbaroni tarehe 6 Novemba mwaka huu katika viwanja vya Bunge Mjini Dodoma, anaandika Wolfram Mwalongo.

Hatimaye Mahakama Kuu, Kanda ya Arusha, imekubali maombi ya mawakili wake (Sheck Mfinanga na Faraji Mangula) ya kuwasilisha notisi ya nia ya kukata rufaa dhidi ya dhamana yake iliyozuiliwa.
Jaji Dk. Modesta Opiyo, anayesikiliza shauri hilo Tarehe 20 (jana) alitoa siku kumi kwa upande wa mshtakiwa huyo, kuwasilisha maombi yake ya dhamana nje ya muda.

Awali Mawakili upande wa Jamhuri (Matenus Marandu na Hashimu Ngole) uliwasilisha pingamizi mbili katika maombi hayo namba 69 ya mwaka huu, ukiiomba mahakama hiyo isisikilize maombi hayo kutokana na kushindwa kufuata taratibu za kisheria.

Desemba 16 mwaka huu, Jaji Dk. Opiyo alitupilia mbali pingamizi hizo na kusema mahakama haioni sababu ya msingi ya kumnyima haki Lema kwa kuwa hoja zilizowasilishwa mahakamani hapo na upande wa wajibu maombi, hazikuwa na mashiko kisheria.

Akisoma uamuzi wake jana, Jaji Dk. Opiyo alisema busara ya mahakama ni kuendelea kutoa haki na inakubali maombi na inampa mleta maombi siku 10 kuanzia jana ili awasilishe maombi yake nje ya muda.

Jaji Dk. Opiyo ambaye alianza kusoma uamuzi huo jana saa 6:26 mchana hadi saa 7:18, hata hivyo alisema kwamba kuondolewa kwa kesi hiyo hakuzuii kuata rufaa nyingine kwakuwa ni haki ya mtuhumiwa.

“Mahakama hii kwa kuzingatia uamuzi wa kesi mbalimbali, ni lazima izingatie na kuangalia sababu, muda na athari ambazo zitatokana na uamuzi wake.

“Mahakama haikubaliani na hoja za upande wa wajibu maombi na imeona ucheleweshwaji wa notisi ya kusudio la kukata rufaa ulikuwa na sababu za msingi, hivyo inakubali maombi haya na inampa mleta maombi siku kumi kuanzia sasa.

“Kwa kuzingatia haki, walichelewa kwa sababu za msingi, hivyo mahakama haijaona kuwa ucheleweshwaji huo ni wa makusudi na katika siku mbili au tatu walizochelewa, kulikuwa na mashauri mengine yaliyokuwa yakiendelea mahakamani,” alisema Jaji Dk. Opiyo.

Hata hivyo Baada ya uamuzi huo, Lema alirudishwa mahabusu akisubiri mawakili wake kufanya taratibu za kupatikana kwa dhama na mahakama ikiridhia Mbunge huyo ataachiwa kwamjibu wa taratibu za dhamana.

Mawakili wa pande zote mbili wamekubaliana na uamzi huo wa mahakama huku wote wakionesha kuridhishwa na hatua iliyoamriwa na mahakama hiyo.

Lema alitiwa mbaroni Novemba 6 mwaka huu katika viwanja vya Bunge Mjini Dodoma na kusafirishwa usiku kwa usiku hadi Arusha, ambapo anatuhumiwa kutoa maneno ya kichochezi.

No comments:

Powered by Blogger.