Trending News>>

Mwakyembe aagiza TFF ifuatilie uonevu ligi daraja la kwanza..

Taarifa kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo inasema kwamba, Waziri mwenye dhamana ya Michezo Dk. Harrison Mwakyembeameshtushwa na kusikitishwa na malalamiko ya wadau wa soka nchini kuhusu vitendo vya uonevu na upendeleo vinavyodaiwa kujitokeza kwa nguvu katika uendeshaji wa michezo ya ligi daraja la kwanzaTanzania bara na ukimya wa Shirikisho la Soka nchini (TFF) katika kufanyia kazi malalamiko hayo ili kujenga afya njema ya mchezo wa soka Tanzania.
Katika salamu zake za mwaka mpya kwa Rais, Makamu wa Rais na Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, Dk. Mwakyembe amewataka viongozi hao kuchukua hatua haraka kuchunguza kilichojiri katika mechi mbili zilizochezwa Jumamosi tarehe 30 Disemba, 2017 kati ya Dodoma FC na Alliance ya Mwanza na kati ya Pamba ya Mwanza na Biashara ya Musoma na kutoa maamuzi ya haki bila kuangalia sura ya mtu ndani ya wiki hii bila kukosa.
“Watanzania wanahaki ya kujua kwa uwazi na ukweli msingi wa kadi nne nyekundu kutolewa kwa wachezaji wa timu moja katika mchezo mmoja, wanataka kujua kama kweli muda halali ulifuatwa kumaliza mchezo kati ya Dodoma na Alliance , wanataka kujua kama kweli waandishi wa habari za michezo walizuiwa kufanya kazi yao ya kikatiba ya kuwataarifu watanzania wenzao kuhusu mmichezo hiyo miwili na kama ni kweli, nani aliwazuia, wanataka kujua kama vitendea kazi vyao viliharibiwa na wahusika walikuwa nani, wanataka kujua kauli za makamisaa wa mechi hizo mbili, wanataka kujua faida ya kuendelea kuwa na Kamati ya Masaa 72 , na wanataka kujua hisia za ujumla za watazamaji siku hiyo kuhusu usimamizi wa michezo hiyo miwili”,Dk. Mwakyembe amesisitiza katika salamu zake hizo za mwaka mpya.
Waziri Mwakyembe amesema pamoja na kwamba dhamana ya kusimamia na kuendeshampira wa migu  imekasimiwa kwa TFF, kama Waziri wa Sekta hiyo hawezi kukaa kimya wakati tuhuma nzito za upendeleo na milungula zinapoibuliwa, wakati TFF haishtuki mara moja na kuchukua hatua za haraka.
“Tukiwa na mfumo mbovu uliosheheni mizengwe katika kupata timu bora za kupanda daraja kuingia ligi kuu, tusahau kuwa ligi kuu yenye msisimko na ushindani mkal”, amesema Waziri Mwakyembe.
Amewakumbusha viongozi wa TFF kuwa watanzania wameupokea uongozi wao kwa imani, shauku na matarajio makubwa, hivyo wasiwavunje moyo kwa kigugumizi cha kujitakia katika maamuzi. Wahakikishe kuwa kila tuhuma inapatiwa maelezo ya kina na dhati, wakianza na tuhuma za upendeleo na uonevu katika mechi mbili alizozitaja.
Amewataka viongozi hao wasipuuze chochote na kudhani watanzania hawajui, la hasha wanajua ila wanawasogezea kamba polepole viongozi hao wajinyonge wenyewe. Mathalani amesema, katika malalamiko waliyomletea toka Jumamosi iliyopita kuhusu mechi hizo mbili, wananchi wanadai uwepo wa kampeni ya makusudi upande wa viongozi wa TFF ya kuifanya timu ya Dodoma iingie ligi kuu kwa udi na uvumba.
“Si dhambi kuiombea timu ya makao makuu ya nchi kuingia ligi kuu, lakini si sahihi hata kidogo kwa viongozi kuibeba timu hiyo kama madai hayo ni sahihi”, amesisitiza.
Aidha, tuhuma zingine ambazo hazina uthibitisho zinauhusisha uongozi wa TFF kuzibeba timu za Coastal Union na timu ya Biashara ya Musoma.

No comments:

Powered by Blogger.