Trending News>>

Mabinti Wanaswa Wizi wa Pikipiki, Sare za Jeshi


JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewakamata watu watatu, wakiwemo mabinti wawili wa miaka 19,  kwa tuhuma za kujihusisha na  wizi wa pikipiki jijini humo.
Hayo yamesemwa leo na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa wakati akizungumza na wanahabari jijini Dar alipokuwa akitoa taarifa ya oparesheni maalum katika kukabiliana na uhalifu.
“Tumekamata watu watatu kwa tuhuma za wizi wa pikipiki lakini miongoni mwao ni mabinti wawili wa miaka 19 ambao wanatuhumiwa kutumika kama chambo ili kufanikisha mazoezi ya wizi na matukio mengine ya uhalifu.
“Pia tumefanikiwa kuwakamata watu wawili wanaodaiwa kuiba sare za jeshi, ambapo wanatuhumiwa kutumia sare hizo kufanya wizi na matukio mbalimbali ya uhalifu,” alisema Mambosasa.
Aidha jeshi hilo litawafikisha mahakamani watuhumiwa hao pindi litakapokamilisha uchunguzi wake.
Akizungumzia kuhusu Sikukuu za Krismasi na Mwaka Mpya, Kamanda Mambosasa amesema:
“Kuelekea msimu huu wa Sikukuu, tumejipanga vizuri kufanya doria, mpaka sasa jiji la Dar liko salama. Niwaonye wahalifu msijidanganye kujaribu kufanya mabo ya ajabu, tuko imara kuhakikisha Sikukuu zinamalizika salama.”
Mambosasa amepiga marufuku  ‘disko toto’ kwa kuwa disko hizo nyingi hazijakidhi vigezo.  Pia amewataka wazazi kufuata njia salama ya kuwafurahisha watoto wao katika siku hiyo ya Sikukuu.
“Tumeamua eneo la Tanganyika Packers, Kawe,  kuwa ni eneo maalum la kusheherekea kipekee Siku ya Mwaka Mpya. Pia ni marufuku mtu kufyatua fataki siku ya Mwaka Mpya. Tutatoa nusu saa tu katika eneo la Tanganyika Packers kuwa sehemu maalum  ya kupiga hizo fataki,” alieleza Mambosasa.

No comments:

Powered by Blogger.