Trending News>>

Dr. Shein: Wala Rushwa CCM Wajadiliwe, Watimuliwe

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi(CCM), Mwekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amewataka viongozi wa chama kutosita kuwajadili wanachama ambao wanakiuka maadili ya chama hususan vitendo vya rushwa.

Pia, amesema wanachama hao wakishajadiliwa hawatasita kufukuzwa ndani ya CCM na kwamba imefikia hatua baadhi ya watu hao ambao wanafanya vitendo hivyo wanaonewa haya.

Hayo ameyasema jana , katika sherehe za kumpongeza kuchaguliwa tena nafasi ya Makamu Mwenyekiti, iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mkoa Mjini ,ambapo aliwataka viongozi hao kutofumbia macho vitendo hivyo ndani ya CCM.

Katika maongezi yake Dk.Shein aliongeza kuwa vitendo hivyo vya rushwa si jambo jipya ndani ya CCM na kwamba inaharibu sana maadili ya chama.

“Vitendo hivi vya rushwa ndani ya CCM si suala jipya lakini tunaoneana huruma, tunafichiana na baadae tunalalamikiana wakati chama ni ya wanachama hivyo lazima tushirikiane,”alisema.

Makamu Mwenyekiti huyo Dk.Shein alisema utaratibu wa chama kinajielekeza wanachama ambao wanakiuka maadili wanapaswa kujadiliwa kuanzia ngazi za tawi na baadae inawasilishwa kwenye uongozi wa juu na kuchukuliwa hatua.

Alieleza chama kipo kwa wanachama ikiwemo kwenye mashina na matawi na taratibu zinafafanua kuwa ngazi hizo ndipo mambo hayo yanazungumzwa kwamba mwanachama akikiuka maadili anajadiliwa kwenye tawi.

“Anajadiliwa kwenye kamati ya tawi na shina, kamati ya jimbo, kamati ya wilaya, Halmashauri ya wilaya ndipo wanapojadiliwa huku kwamba anafaa ama hafai hachukuliwe hatua za kufukuzwa ama asichukuliwe,”alisema.

Makamu Mwenyekiti huyo alisema utaratibu unaeleza kuwa baada ya kujadiliwa wanachama hao taarifa itapelekwa kwenye ngazi za juu na kufanya maamuzi ya kumfukuza.

“Nachotaka kueleza kuwa kazi hii ni ya wote na kwamba jukumu kubwa ni kuhakikisha CCM inashinda mwaka 2020 msiwafiche watu ambao wanataka kuharibu chama, na kwa kufanya hivyo ni sawa na kuwa ndumi la kuhili tunayoyasema sio tunayoyafanya,”alisema  Makamu Mwenyekiti.

Alifafanua kuwa kazi ya siasa ya kipindi hiki lazima kuongeza kasi ambapo kuna mambo zaidi ya kuyafanya na hata Mwenyekiti Dk.John Magufuli alisisitiza kwenye mkutano mkuu uliofanyika Desemba 18, mwaka huu mjini Dodoma.

Mbali na hilo, Dk.Shein aliwataka viongozi wa serikali kutambua na kuheshimu CCM kutokana na kuwa wanafanya kazi ya utekelezaji wa chama hivyo hawanabudi kukithamni.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Dk.Abdallah Juma Saadalla(Mabodi), alisema wanachama kutoka visiwani humo wanatarajia kusimamia vyema ibara ya tano ya kuhakikisha CCM inashinda mwaka 2020.

Aliongeza kuwa uchaguzi uliopita ulikuwa na mawimbi makubwa sana lakini watu walioshiriki walikuwa wanastahili.

“Bado tunafanya juhudi za kutoa elimu kwa viongozi wa chama kuhusu suala la kuzingatia kanuni na maadili ili kuhakikisha wanasongesha gurudu la uchaguzi wa mwaka 2020″alisema.

Dk.Mabodi ameeleza  kuwa anamshukuru Mungu kwa kuwa wagombea wote ambao wamepita kwenye uchaguzi huo asilimia kubwa wana maadili ya kutosha.

No comments:

Powered by Blogger.