Wauaji wilayani Kibiti wadaiwa kutuma ujumbe kuwa wataendelea kuwauawa Polisi kwa sababu huwadhulum
Siku
 mbili tangu kuuawa kwa polisi wawili wa Kikosi cha Usalama Barabarani 
ambao walikuwa kazini katika Kijiji cha Bungu B, hali ya wasiwasi 
imezidi baada ya wauaji hao kusambaza ujumbe unaoeleza kuwa wanaendelea 
kusaka askari kwa kuwa ni wadhurumaji.
Watu
 hao wametuma ujumbe mfupi uliondikwa kwenye karatasi na kisha kuutuma 
katika mitandao ya kijamii, ukidai kuwa waliouawa (japo hawajatajwa 
majina yao) walidhulumu watu kwa kutumia kazi zao.
“Tunawatangazia
 wananchi tumewaua hawa kwa sababu wanadhulumu watu kwa kutumia kazi zao
 na yeyote atakayefanya kazi hapa au nje ya hapa tutamtafuta hata 
nyumbani kwake. Sisi tumejitolea kufa kuliko kuishi, kwa hiyo dereva au 
raia popote uwaonapo toa taarifa iwe nyumbani au kazini,” unasema ujumbe huo.
“Hakuna njia ya kumaliza dhuluma isipokuwa chuma tu, hapa chuma tuuu!”
Ujumbe
 huo ambao umeandikwa kwa mkono kwa kutumia kalamu ya rangi ya bluu 
unadaiwa kuwa unazungumzia vifo vya askari polisi wawili wa Kituo cha 
Polisi Kibiti, Sajent Salum na PC Masola waliouawa kwa kupigwa risasi 
wakiwa kazini.
Mmoja
 wa madiwani katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti (jina tunalo) 
alisema ujumbe huo unawalenga askari wa kawaida na wa Kikosi cha Usalama
 Barabarani.
Diwani huyo alisema kundi hilo linalofanya mauaji katika wilaya za Kibiti na Rufiji bado lipo na lina nguvu.
“Linaonyesha bado lina uwezo mkubwa wa kufanya mauaji na kutokomea kusikojulikana,” alisema.
Alisema
 kwa sasa Serikali inapaswa kuongeza nguvu zaidi ya wapelelezi ili 
kukomesha kikundi hicho ambacho hakijajulikana kinafanya hivyo kwa 
sababu zipi na wala kinakojificha.
Akizungumzia ujumbe huo, kamanda wa polisi wa Pwani, Onesmo Lyanga alisema Jeshi la Polisi litaendelea kuwasaka.
“Tutapambana nao tu,” alisema Kamanda Lyanga na kukata simu.
Chanzo: Mwananchi 

No comments:
Post a Comment