Singida United yachekelea SportPesa Super Cup
 Kocha msaidizi wa Singida 
United Fred Minziro amesema mashindano ya SportPesa Super Cup 
yanayotarajiwa kuanza kutimua vumbi kuanzia Juni 05 mwaka huu ni kipimo 
kizuri kwa timu yake kwa ajili ya maandalizi ya kuelekea katika msimu 
ujao wa ligi kuu. 
Kocha msaidizi wa Singida United, Fred Minziro
Kocha
 Minziro amesema, mashindano hayo yatakuwa na ushindani mkubwa kutokana 
na kushirikisha timu kutoka Kenya, Zanzibar na Tanzania Bara ambapo 
ameongeza kuwa anaamini kikosi chake kitafanya vizuri kutokana na 
usajili uliofanyika.
"Haya mashindano ni makubwa 
lakini kwa upande wetu yamekuwa kama yakushtukiza lakini ni makubwa na 
yatakuwa na ushindani mkubwa na kwa upande wetu yatakuwa mazuri kwani 
yatasaidia kujua mwanzo tunapoanza na tunapoelekea katika Ligi," amesema Kocha Minziro.
Minziro amewataka Wanasingida kuona mambo mazuri katika mashindano ya SportPesa pamoja na Ligi Kuu Tanzania Bara kwa ujumla.
"Kwa ujumla Wanasingida 
wategemee mazuri kwasababu hata usajili wanausikia na tuangalie Jumatatu
 ambapo tutaanza kuingia katika hayo mashindano ndipo tutajua timu 
inaelekea wapi, " amesema Minziro.
Naye Katibu mkuu wa Singida United 
Abrahman Sima amesema, kikosi kipo kamili kwaajili ya mashindano hayo 
huku akiongeza kuwa mpaka sasa wameshawasajili wachezaji watano wa 
kimataifa na wanategemea kuwa na wachezaji saba kabla ya kuanza kwa Ligi
 kuu ya Soka Tanzania Bara msimu ujao.
"Nwapongeza SportPesa kwa 
kutupatia nafasi kama hii na timu ipo kambini. Tumeanza mazoezi jana 
rasmi na Wanasingida waamini timu yao itaanza vizuri japo vilabu 
tutakavyokutana navyo vimetoka kwenye Ligi lakini naamini aina ya 
wachezaji tuliokuwa nao tutafanya vizuri katika mashindano ya SportPesa,
 " amesema Abrahman Sima.
Sima amekanusha pia kuingia usajili na 
wachezaji wa ndani Deus Kaseke wa Yanga na Ibrahim Ajibu wa Simba SC 
ambapo ameongeza kuwa kwa sasa wachezaji wa kimataifa ni watano na lengo
 lao ni kuwa na wachezaji saba.
"Kwa wachezaji wa ndani 
mpaka sasa tuliofanya makubaliano nao ni Kenny Ally ambaye ataingia 
kesho, tuna Atupele Green na ameshawasili pamoja na Salum Chuku lakini 
hao wengine sio kweli lakini ikitokea wakawepo hapo baadaye tutawaambia,
 " amesema Sima.
 
No comments:
Post a Comment