Trending News>>

Wizara ya Maliasili na Utalii kutoa miche Laki Saba kampeni ya Dodoma ya Kijani

Wizara ya Maliasili na Utalii imeeleza kwamba inatarajia kutoa miche ya miti zaidi ya Laki Sita ambayo itatumika kupandwa katika Wilaya zote za Mkoa wa Dodoma kuunga mkono kampeni ya ‘Dodoma ya Kijani’  yenye kauli mbiu (Dodoma ya Kijani ndio mpango mzima) iliyozinduliwa rasmi leo Desemba 21,2017 na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ambaye alikuwa mgeni rasmi tukio lililofanyika katika kijiji cha Mzakwe nje kidogo ya Manispaa ya Dodoma.
Akizungumza katika uzinduzi wa kampeni hiyo Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla alisema kuwa Wizara yake kwa kuanzia wanatoa miche ya miti Laki moja ambayo itapandwa kwa Manispaa ya Dodoma na kisha watatoa miche mingine Laki Sita ambayo itaenda kwenye  Wilaya zote za Mkoa  huo wa Dodoma.
“Napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutufikisha salama kwneye tukio hili muhimu, Ni ukweli usiopingika kwamba Dodoma ni makao makuu ya nchi yetu.  Na sote tunao wajibu wa kuifanya Dodoma ipendeze  na ya kuvutia.
Mazingira ya Dodoma yakiboreshwa yatafanya maisha ya wakazi wake kuwa bora pia. Mheshimiwa Makamu wa Rais wizara yangu, Kama munavtofahamu, inayo wajibu mkubwa wa kulinda, kudumisha na kuhifadhi maliasili zetu, hususani wanyama pori na misitu hivyo  tutaungana bega kwa bega katika program hii ya kudumu na kuifanya Dodoma kuwa ya Kijani” alieleza Dk. Kigwangalla.
Aidha, Dk. Kigwangalla alimweleza Makamu wa Rais, kuwa  wizara hiyo inayo wajibu wa kuendeleza Utalii nchini, hivyo itaungana nae katika mpango huo kwani upanndaji wa miti usaidia uhifadhi wa viumbe hai hususani mimea ambayo ufanya uso wa dunia kupendeza na kuwa na afya na kuwezesha kutoa huduma zake za kiikolojia vizuri zaidi ambazo ni pamoja na hewa safi, maji,  kuvutia mvua na mambo mengine mengi yatokanayo na faida za kupanda miti.
“Makamu wa rais, tunapoungana leo katika zoezi hili tunaendeleza dhana yetu pana kama wizara na kama taifa katika kuifanya Dodoma kuwa ya kijani ili linawezekana na tutahamasisha na miche hii itakayotolewa itakuwa chachu zaidi. Pia wizara yangu itafanya iendelee kuzalisha miche zaidi ya kupandwa ili kulinda uoto wa nchi yetu hasa maeneo makame kama haya ya Mkoa wa Dodoma.” Alimalizia Dk.Kigwangalla.
Awali akisoma hutuba wakati wa ufunguzi rasmi wa tukio hilo, Makamu wa Rais Samia  Suluhu Hassani, amewaagiza wakuu wa mikoa yote nchini kusimamia programu ya upandaji miti pamoja na Halmashauri zote kutunga sheria ndogondogo zitakazo elekeza kila shule, vyuo, familia na taasisi mbalimbali kupanda miti na kuitunza katika maeneo yao.
Makamu wa Rais amebaainisha kuwa, kuwa Takwimu zinaonyesha takribani asilimia 61 ya nchi iko hatarini kuwa jangwa kutokana na vitendo vya uharibifu wa mazingia unaofanywa na shughuli mbalimbali za kibinadamu.
“Kutokana na uharibifu wa mazingira ikiwa ni pamoja na suala la ukataji miti hovyo kumeongeza migogoro baina ya wafugaji na wakulima kutokana na eneo la malisho kupungua hali ambayo sisi kama taifa inatakiwa tuwekeze nguvu zetu katika upandaji miti ya kutosha” alisema Samia.
Pia amebainisha kuwa, kutokana na mabadiliko ya tabia ya nchi watanzania hawana budi kupanda miti kwa wingi ili kuweza kurudisha uoto wa asili utakaosaidia kuongeza mvua pamoja na kupunguza ongezeko la joto Duniani.
“Sheria ya mazingira ya mwaka 2004 ipo na inakemea vitendo vya uharibifu wa mazingira ambavyo vimekuwa vikifanywa na watu mbalimbali lakini pia ipo mikakati mbalimbali ya serikali kama ile ya kupamna na hali ya jangwa ambazo zote hizi zinaonyesha ni kwa umuhimu gani suala la mazingira ni muhimu”alisema.
Akielezea sheria,  ameweka wazi kuwa, suala la uvunaji wa miti lizingatie sheria kanuni na taratibu ili kusiwe na tatizo la kukata miti bila kupanda miti mingine.

No comments:

Powered by Blogger.