Trending News>>

Simba yapata pigo hili


AFISA HABARI WA KLABU HIYO, HAJI MANARA.
ZIKIWA zimebaki siku tisa kabla ya mchezo wao muhimu dhidi ya Yanga Oktoba 28, mwaka huu, benchi la ufundi la Simba limepata pigo baada ya kuthibitika kuwa beki wao tegemeo, Salim Mbonde na mshambuliaji John Bocco wataukosa mchezo huo.

Mbonde aliyeumia kwenye mchezo uliopita dhidi ya Mtibwa Sugar kama ilivyo kwa Bocco, atakuwa nje kwa zaidi ya wiki nne kufuatia majeraha ya goti aliyoyapata huku Bocco akitarajiwa kuwa nje kwa wiki moja.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Afisa Habari wa klabu hiyo, Haji Manara, alisema kuumia kwa wachezaji wao ni pigo, lakini wanajivunia upana wa kikosi chao.

“Wachezaji wote hawa ni muhimu kwetu na ni pigo kwetu ukizingatia tuna michezo muhimu sana, lakini benchi la ufundi linajivunia ukubwa wa kikosi chetu uliotokana na usajili mzuri tulioufanya,” alisema Manara.

Alisema wakati Bocco ataukosa mchezo ujao dhidi ya Njombe Mji utakaochezwa Jumapili kwenye Uwanja wa Uhuru, Mbonde ambaye amekuwa muhimili mkubwa kwenye safu ya ulinzi ya Simba msimu huu, atakosa michezo dhidi ya Njombe Mji, Yanga na michezo miwili jijini Mbeya dhidi ya Mbeya City na Tanzania Prisons.

Aidha, Manara alisema kuwa golikipa wao aliyekuwa India kwa matibabu, Saidi Mohamed ‘Nduda’, atakuwa nje ya uwanja kwa wiki nne baada ya kufanyiwa upasuaji mara mbili akiwa nchini humo.

“Alipokwenda India alikuwa na tatizo moja, lakini wakati wanamfanyia uchunguzi kabla ya kutibu tatizo lake, waligundua tatizo lingine ambalo alikuwa nalo kwa muda mrefu, hivyo wakaamua kumfanyia upasuaji kwa ajili ya tatizo hilo, sasa ukiunganisha na upasuaji wa tatizo hilo la pili, Nduda atakuwa nje kwa wiki nne na tunategemea atarejea mwanzoni mwa Desemba,” alisema Manara.

Pia, alisema beki wao Shomari Kapombe naye amepewa muda zaidi wa kupumzika ili kuimarika zaidi.

Simba inayodhaminiwa na Kampuni ya Kubashiri Matokeo ya SportPesa ka iliyo Yanga, leo inaanza mazoezi kujiandaa na mchezo dhidi ya Njombe Mji baada ya mapumziko ya siku mbili.

No comments:

Powered by Blogger.