Trending News>>

Watano wafariki katika matukio mawili tofauti


WATU watano wakazi wa Wilaya ya Tarime mkoani Mara wamefariki dunia katika matukio matatu tofauti juzi na jana watatu wakigongwa na gari na wengine kuchomwa visu sehemu mbalimbali.

Waliogongwa na gari ni Bhoke Burure (22) mkazi wa Kijiji cha Magena na Chacha Marwa mwendesha bodaboda yenye namba za usajili MC722 AYU aina ya Sun LG wa Kijiji cha Itebe Magena. Mwingine ni mwendesha baiskeli ambaye jina halikufahamika. Waligongwa na gari aina ya Probox yenye namba T358 DHV iliyokuwa ikiendeshwa na John Mangera.

Pia wanawake Bhoke Chacha (30) mkazi wa Kijiji cha Magoma na Ghati Mwita (24) wa Kijiji cha Mogabiri waliuawa kwa kuchinjwa na mwingine kwa kuchomwa visu sehemu mbalimbali za mwili. Umati mkubwa wa wananchi ulifika kuona na kutambua miili ya marehemu hao katika hospitali ya wilaya Tarime. Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dk Mkumbo Luther alikiri kupokea miili hiyo.

“Tumepokea miili ya watu watano jana (juzi). Ipo hapa chumba cha maiti, minne kati yake imetambuliwa na ndugu zake. Marehemu waliotambuliwa ni wa ajali ya gari iliyotokea mchana katika Kijiji cha Magena Kata ya Nkende. Waliotambuliwa ni Bhoke Burure mkazi wa Kijiji cha Magena aliyekuwa mjamzito, na mwendesha bodaboda, Chacha Marwa mkazi wa Kijiji cha Magena,” alisema.

Aliwataja marehemu wengine kuwa ni ya kijana wa miaka kati ya 20 - 25 ambaye hajatambuliwa jina lake na makazi yake, wanawake Bhoke Chacha aliyekutwa ameuawa kwa kuchinjwa shingo na mwili wake kutupwa kando ya barabara itokayo Nyamwigura na Mogabiri na Ghati Mwita aliyeuawa Kijiji cha Nyangoto Nyamongo kwa kuchomwa visu sehemu mbalimbali za mwili wake.

Aliwataja majeruhi wawili waliolazwa kutokana na kujeruhiwa katika tukio hilo kuwa ni mwanafunzi wa Shule ya Msingi Magena, Frank Mwita (12) aliyeumia sehemu mbalimbali za mwili na mwanamke raia wa Kenya, Carelin Adhiambo kutoka Rongo Mkoa wa Nyanza ambaye amejeruhiwa mgongoni.

Kaimu Kamanda wa Polisi wa Tarime/Rorya, Sweetbert Njewike alithibitisha kutokea kwa ajali hizo. Alisema dereva na mmiliki wa gari la Probox lililosababisha ajali hiyo, John Mangera alitoroka na anaendelea kutafutwa huku uchunguzi ukifanywa kuhusu mauaji ya wanawake hao.

No comments:

Powered by Blogger.