Trending News>>

Megawati 100 umeme upepo kuanza Singida mwakani:


UMEME wa upepo wa megawati 100 unatarajiwa kuanza rasmi mwakani mkoani Singida hivyo kuwanufaisha wakazi wake.

Mwanzilishi wa Kampuni ya Six Telecoms, Rashid Shamte alisema hayo alipozungumza na gazeti hili Dar es Salaam.

Mbali na kampuni hiyo kupitia kampuni yake tanzu ya Wind East Afrika, kampuni nyingine mshirika wa mradi huo ni Aldwych International ya Uingereza na Taasisi ya Fedha ya Benki ya Dunia (IFC).

Shamte alisema mradi huo utawanufaisha wakazi wengi wa mkoa huo kwa upande wa biashara na ajira pamoja na kuchangia megawati 100 katika Gridi ya Taifa ya umeme.

“Wawekezaji wengi watawekeza katika mkoa huo kutokana na upatikanaji wa uhakika wa umeme na hivyo kuufanya mkoa huo kupata maendeleo makubwa na kukua kimji,” alisema Shamte na kuongeza kuwa mbali ya kuanza kwa uzalishaji huo rasmi, lengo ni kuanza uzalishaji mapema ili kufikia malengo yao ya kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na vile vile kuunga mkono kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli ya Tanzania ya viwanda.

“Kwa sasa tumetangaza zabuni kwa ajili ya ununuzi wa mitambo, zabuni hii itafungwa mwezi Mei na baada ya kupata mzabuni, tutaanza mikakati ya kulipa fidia wakazi waliopo katika eneo la mradi, lengo ni kuona mpaka Septemba, eneo hilo litakuwa tayari kwa ujenzi na kufunga mitambo.

“Mradi huu unafadhiliwa na Benki ya Dunia kupitia taasisi yake ya IFC, nawaomba wakazi wa Mkoa wa Singida kuwa tayari kwa mabadiliko na ninadhani kupitia mradi huu, mji utaongeza hadhi yake,” alisema Shamte.

No comments:

Powered by Blogger.