Trending News>>

Yanga Yamtema Rasmi Mbuyu Twite

Mchezaji kiraka wa mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara Dar Young Africans, Mbuyu Twite ametemwa rasmi katika klabu hiyo baada ya mkataba wake kumalizika.

Akithibitisha taarifa hizo, Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga, Baraka Deusdedith, amesema mkataba wa kiungo huyo ambaye mara nyingine hucheza kama mlinzi wa pembeni unamalizika mwezi huu, na tayari walikwishafanya naye mazungumzo kuwa hawata endelea naye.

Baraka amesema sababu kuu ya kumtema nyota huyo raia wa DRC ni kutokana na Yanga kumpata mbadala wake, ambaye ni Justine Zulu kutoka Zambia na kwamba kumuacha Mbuyu hakumaanishi kuwa hana kiwango, isipokuwa ni kupatikana kwa mbadala wake.

Mbuyu Twite baada ya kuwasili nchini Mwaka 2012 na kuvalishwa jezi yenye namba sawa na jezi aliyokuwa ameandaliwa Simba na kutangazwa na mwenyekiti wake enzi hizo, Ismail Rage

Awali palikuwa na tetesi kuwa huenda mchezaji huyo aliyejiunga Yanga mwaka 2012 akitokea APR ya Rwanda akatua kwa mahasimu wao Simba Sc, jambo ambalo Baraka amesema wanamtakia kila la kheri kokote atakapokwenda.

Ujio wa Mbuyu nchini Tanzania mwezi August mwaka 2012 ulitikisa anga la usajili katika vilabu vya Simba na Yanga kutokana na kuwaniwa na vilabu vyote viwili huku Simba wakidai kuwa walikwisha mlipa pesa za usajili, lakini akaangukia Jangwani na kukumbana na mapokezi ya aina yake katika uwanja wa ndege wa Dar es salaam.

No comments:

Powered by Blogger.