Trending News>>

Meya Mbaroni Kwa Kuchoma Msitu


POLISI mkoani Rukwa inamshikilia Meya wa Manispaa ya Sumbawanga, Justine Maliwasa (CCM) akituhumiwa kuhusika na kuteketezwa kwa moto msitu wa hifadhi wa Mbizi na kusababishia serikali hasara ya zaidi ya Sh milioni 226.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Rukwa, George Kyando amethibitishwa kuwa mwanasiasa huyo alikamatwa juzi na kuhojiwa kwa saa kadhaa.

“Kweli (Maliwasa) amehojiwa lakini ni mahojiano tu yanayoendelea, taarifa zaidi itatolewa hadharani baadaye kwa sasa bado anahojiwa.

“Anahojiwa baada ya watuhumiwa tuliowakamata kwa kosa la kuteketeza msitu huo wa hifadhi kwa moto walipodai kuwa wametumwa na Meya huyo (Maliwasa),“ alisisitiza.

Taarifa kutoka ndani ya jeshi hilo zinaeleza kuwa mwanasiasa huyo ambaye ni Diwani wa Kata ya Senga katika Manispaa ya Sumbawanga, alihojiwa katika Kituo Kikuu cha Polisi mjini hapa kuanzia saa tano asubuhi hadi usiku.

Msitu huo ni chanzo kikubwa cha maji cha wakazi wa mji wa Sumbawanga na vitongoji vyake kwa asilimia 80.

Msitu huo wenye ukubwa wa ekari 1,260 ambao umepandwa miche ya miti mwaka 2014, unasimamiwa na Mamlaka ya Huduma za Misitu (TFS).

No comments:

Powered by Blogger.